Wizara Yaendesha Mafunzo
Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika imeendesha mafunzo ya usimamizi na uhifadhi wa zao la mpunga baada ya mavuno, yaliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Edema katika Manispaa Morogoro kuanzia tarehe 20 – 31 Januari, 2014.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Idara ya Zana Eng. Mark Lyimo, Mafunzo hayo yaliwwahusisha Maafisa Zana na Ugani wapatao 14 na wakulima 84 kutoka skimu 14 za umwagiliaji wa Halmashauri za Mikoa ya Mbeya, Morogoro, Tanga, Arusha, Iringa, Kilimanjaro Manyara na Ruvuma.
Pia katika mafunzo haya taasisi binafsi ya RUDI ilishiriki ikiwa ni katika harakati za kushirikisha sekta binafsi katika kuboresha kiilimo hapa nchini.
Baadhi ya mada zilizowasilishwa katika mafunzo haya ni pamoja na uzalishaji kitaalam, usindikaji wa zao la mpunga na kanuni zake, Uhifadhi bora wa zao la mpunga, ufungashaji na kupiga chapa bidhaa za mpunga katika kulenga soko, alifafanua Eng. Lyimo.
“Lengo kubwa la mafunzo haya ni kutoa elimu kwa maafisa zana na wakulima kwenye skimu za umwagiliaji ili waweze kutumia teknolojia za kisasa katika kuzalisha, kuvuna na kuhifadhi katika kuongeza thamani kwa lengo la kuboresha na kuongeza tija kwa mkulima mdogo katika maeneo ya umwagiliaji hapa nchini” aliongeza Eng. Lyimo.
Mada nyingine ni kanuni bora za uzalishaji wa zao la mpunga, usindikaji, matumizi sahihi ya mashine bora katika kilimo cha mpunga zitakazotolewa na Serikali katika skimu 14 chini ya Mradi wa Sera na Maendeleo ya Rasilimali Watu (PHRD), alifafanua Eng. Lyimo.
Mafunzo haya ni sehemu ya utakelezaji wa mpango wa Serikali wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) kwa Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika ambapo zao la mpunga ni mojawapo linalopewa kipaumbele katika kuongeza uzalishaji na tija.