Skip to main content
Habari na Matukio

Chiza Ainisha Fursa za Kilimo

Waziri wa Kilimo Chakula na Ushirika Mhe. Eng. Christopher Kajoro Chiza ameainisha fursa za kilimo ambazo inaweza kushirikiana na serikali ya Uturuki katika kuinua kilimo hapa nchini.

Eng. Chiza aliyasema hayo wakati akizungumza na ujumbe maalumu kutoka  Uturuki ukiongozwa na Waziri wa Kilimo Chakula na Ushirika Mhe. Mehdi Eker, ambao ulifika Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika kubadilishana mawazo katika kushirikiana uboreshaji wa kilimo.

Moja ya fursa alizobainisha ni pamoja na uwekezaji wa sekta binafsi katika kilimo, sekta ambayo bado haijafanya vya kutosha katika kuinua kilimo.

“Tanzania ina eneo kubwa la kuwekeza katika kilimo lakini bado sekta binafsi haijachukua nafasi yake katika kuinua kilimo” aliongeza Eng. Chiza

Miundo mbinu katika kilimo cha umwagiliaji maji ni sehemu moja ambayo serikali ya Tanzania inaweza kushirikiana na Uturuki na watu wake katika kuboresha kilimo hapa nchini kwa kujenga miundo mbinu bora katika kilimo.

“Bado nchi yetu ina miundo mbinu hafifu  ya teknolojia ya matumizi ya maji katika kuinua kilimo hapa nchini” alifahamisha Eng. Chiza.

Mheshimiwa Eng. Chiza aliitaka pia serikali ya Uturuki kushirikiana na Tanzania katika kuanzisha mpango kabambe wa kuwashirikisha vijana wa Tanzania katika kuinua kilimo hapa nchini.

“ Vijana wetu wanahitaji kupewa moyo ili washiriki kikamilifu katika shughuli za kilimo ili kweli tuweze kufanikiwa katika kilimo chetu kwani vijana ndio nguvu kazi,” aliainisha Mhe. Chiza.

Eneo lingine ambalo Mhe. Eng. Chiza aliuambia ujumbe wa Uturuki kuweza kushirikiana na Tanzania ni kilimo cha maua.

Aliongeza kuwa mfumo wa usafirishaji wa bidhaa za maua hadi katika soko lake bado ni tatizo nchini kwetu, hinyo aliomba Uturuki kushirikiana na Tanzania katika eneo hili ili kuinua kilimo hiki.

Mbali ya fursa hizo pia  Mhe. Eng. Chiza pia aliwafahamisha wajumbe kuwa matumizi ya zana bora za kilimo bado ni kiwango cha chini sana, kwani ni wakulima asilimia 10 tu wanatumia zana bora katika kilimo zikiwemo tractor.

Awali aliwafahamisha  wajumbe hao kuwa   Tanzania ina eneo zaidi ya   milinoni 44  linalofaa kwa kilimo lakini ni asilimia 25 tu linatumika.

Serikali ya Uturuki kupitia ujumbe huo  imeonyesha nia ya kushirikiana Tanzania katika sekta ya umwagiliaji, uzalishaji wa mbegu na kuwekeza katika uzalishaji wa mbolea.

Maeneo mengine ambayo serikali ya Uturuki  imesema kuwa iko tayari kufanya kazi kwa kushirikiana na  serikali ya Tanzania kuwa ni eneo la afya ya mimea, kilimo cha maua na mifugo.

Maamuzi yaliyofikiwa katika mkutano huo ni kuunda kamati maalumu kwa kushirikisha watalaamu wa Tanzania na Uturuki ili kuchambua na kuona maeneo ya kushirikiana katika kuinua kilimo.