Skip to main content
Habari na Matukio

SERIKALI YA DKT. JOHN POMBE MAGUFULI YATOA KIASI CHA BILIONI 78 ILI KUDHIBITI SUMUKUVU – KATIBU MKUU

Serikali ya Rais, Dkt. John Pombe Magufuli imetoa kiasi cha Dola za Marekani milioni 35.3 sawa na bilioni 78 fedha Kitanzania kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi wa Kudhibiti Sumukuvu nchini (Tanzania Prevention for Afflatoxin Contamination - TANPAC).

Sumukuvu inatokana na fangasi wanaoota kwenye mazao ya chakula hususan mahindi na karanga, ambapo fedha hizo zitatumika kujenga miundombinu mbalimbali, ikiwemo maghala katika Halmashauri 14 Tanzania Bara na Zanzibar.

Akizungumza kabla ya kutembelea eneo litakalojengwa ghala la kuhifadhia mazao ya chakula katika kijijini cha Ikindilo wilayani Itilima mkoani Simiyu, Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Bwana Gerald Kusaya anasema fedha hizo zitatumika kujenga maabara mahususi ya kilimo Jijini, Dodoma; Kituo cha karantini ya utafiti wa Sumukuvu, Kibaha mkoani Pwani pamoja na Kituo mahili cha mazao eneo la Mtanana, mkoani Dodoma.

Aidha, Katibu Mkuu Kusaya amesema kupitia mradi wa TANPAC Serikali itajenga Maghala 14 kwa ajili ya kuhifadhi mazao ya chakula aina ya nafaka na kutumia fursa hiyo kuziomba Halmashauri hizo 12 (Tanzania Bara) na mbili Zanzibar kutoa maeneo ambayo hayatakuwa na migogoro ya ardhi ili maghala hayo yajengwe mara moja.

Katibu Mkuu Kusaya ameongeza kuwa thamani ya kila ghala, litakalojengwa katika Halmashuri kila Halmashauri; Litagharimu kiasi cha shilingi milioni 480 na kuongeza kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kumkomboa Mkulima kutokana na changamoto ya sumukuvu ambayo ina athari kubwa kwa afya za walaji pamoja na biashara ya mazao ya kilimo ndani na nje ya nchi.

“Nawaomba Wakurugenzi wa Halmashauri, Wakuu wa Wilaya, Wakulima na Wananchi ambao Halmashauri zao zimepata fursa ya kujengewa maghala haya, waridhie na wataoe maeneo ambayo hayana migogoro ili mwezi Disemba, 2020 tuanze ujenzi, fedha ipo tayari na mchakato wa kuwapata Wazabuni upo kwenye hatua ya mwisho.” Amekaririwa Katibu Mkuu Kilimo, Bwana Gerald Kusaya.

MWISHO!