Skip to main content
Habari na Matukio

DKT TIZEBA AZINDUA AINA MPYA 9 ZA MBEGU BORA ZA MAHARAGE

Waziri wa Kilimo Mhe Dkt. Charles Tizeba leo 20 Juni 2018 amezindua aina mpya Tisa za mbegu bora za maharage katika hafla iliyofanyika kwenye eneo la Taasisi ya utafiti wa Kilimo na Maendeleo Kanda ya Kaskazini (Selian) Mkoani Arusha.

 

Akizungumza katika sherehe hizo, Mhe Tizeba ameitaja Wizara ya Kilimo kupitia taasisi za utafiti wa Kilimo Selian, Uyole na Maruku zikishirikiana na taasisi ya kimataifa PABRA/CIAT ndizo zimegundua mbegu bora hizo tisa za maharage zenye kuongeza uzalishaji na pato la mkulima.

 

Alisema kuwa kati ya hizo aina tisa za  mbegu za maharage, aina mbili zina viwango vya juu vya Madini muhimu ya Zinki na chuma yatakayosaidia kuongeza damu mwilini hasa kwa watoto, mama wajawazito na wazee, ambapo aina nne ni maharage ya muda mfupi yenye kustahimili ukame hivyo kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi huku akizitaja aina zingine tatu kuwa ni kwa ajili ya usindikaji.

 

Alisema kuwa aina hizi Tatu za usindikaji zitawasaidia walaji kuokoa muda wa maandalizi pia itafungua fursa ya uanzishwaji wa viwanda vya usindikaji hivyo kuongeza ajira na kipato kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

 

"Mbegu hizi zitakuwa mkombozi mkubwa katika kuboresha lishe kwenye jamii, kwani tatizo la upungufu wa damu ni tishio kwa watoto na kina mama wajawazito, Aidha ugunduzi juu utachangia kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi kwani kati ya aina zilizogunduliwa kuna zinazokomaa kwa muda mfupi wa kuanzia siku 72" Alikaririwa Dkt Tizeba

 

Mhe. Dkt Tizeba alisisitiza kuwa maharage ni zao muhimu kwa chakula nchini Tanzania na ni zao la pili kwa umuhimu baada ya mahindi hivyo linapaswa kulimwa kwa muktadha wa kibiashara sio kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya familia pekee ambapo pia, alisema kuwa inapaswa kuwekwa juhudi mahususi katika kusambaza aina hizo mpya za mbegu.

 

Katika hatua nyingine, Mhe Dkt. Tizeba amemuagiza Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya utafiti wa Kilimo na Maendeleo Kanda ya kaskazini Ndg Ramadhan Ngatoluwa kukaa upya na watafiti hao ili kuwa na majina mapya yatakayotambua kazi kubwa iliyofanywa na watafiti hao.