Skip to main content

MAKABIDHIANO YA OFISI

Aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo ambaye sasa ni Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Gerald Kusaya  jana (14.04.2021)  amekabidhi rasmi ofisi kwa Katibu Mkuu mpya wa Wizara ya Kilimo Bw. Andrew Massawe  halfa iliyofanyika Dodoma kufuatia mabadiliko yaliyofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan hapo April 04 mwaka huu.

Akizungumza kwenye kikao kilichohudhuriwa na Menejimenti ya Wizara Kamishna Jenerali Kusaya alisema serikali ya Awamu ya Sita imepanga kuona kilimo kinakuwa na mchango mkubwa kwenye upatikanaji ajira na kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi.

"Kilimo ni ajira,kilimo ni biashara hivyo wakulima waendelee kujikita kwa bidii huku wakizingatia matumizi ya kanuni bora  za kilimo na matumizi ya mbegu na pembejeo za Bora" alisisitiza Kusaya.

Kuhusu mapambano ya Kudhibiti Dawa za Kulevya Kamishna Jenerali Kusaya ametoa wito kwa wakulima na wananchi kushirikiana na serikali kwa kuwafichua wote wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya ikiwemo bangi na mirungi ambayo inaathiri maisha ya vijana ambao ni nguvu kazi .

Kusaya alisema " tujione kuwa tuko ndani ya vita,tubebe silaha ili kudhibiti dawa za kulevya ambazo zinaathiri vijana wenye nguvu za kutenda kazi " na kuwa Mamlaka yake imedhamiria kuona biashara hii haramu inadhibitiwa.

Kwa upande wake Katibu Mkuu mpya Wizara ya Kilimo Bw. Andrew Massawe alisema atahakikisha kazi zilizopangwa ikiwemo miradi ya kuwezesha wakulima kunufaika na kilimo inatekelezwa kwa ufanisi .

Massawe ameongeza kusema kipaumbele chake ni kuona Wizara ya Kilimo ikipeleka teknolojia ya kisasa kwenye uzalishaji wa mazao ya wakulima ikiwemo mifumo ya kurahisha utatuzi wa kero .

"Wizara hii ni  inabeba  kundi kubwa la Watanzania ambapo kilimo ndio uti wa mgongo wa uchumi hivyo nitahakikisha elimu inawafikia wakulima waongeze uzalishaji na tija kwenye kilimo" alisema Massawe.