Wataalamu wa Kilimo Wametakiwa Kuwa na Tabia Ya Kusoma Vitabu
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Prof Siza Tumbo amewataka watumishi na wataalamu wa wizara hiyo kujenga tabia ya kujisomea vitabu ili kuongeza uelewa utakaowasaidia katika kuendesha kazi zao za kiushauri .
Akiongea wakati wa kikao kazi kilichofanyika katika Ukumbi wa Kilimo IV hivi karibuni cha kupitia maudhui ya Kitabu kilichoandaliwa kwa ushirikianao baina ya Andrew Coulson, Antony Ellimani na Emmanuel Mbiha kutoka SUA Naibu Katibu Mkuu Prof Siza Tumbo amesisitizia wataalamu wa kilimo kuwa na tabia ya kujisomea vitabu ili kuongeza ujuzi kwa kuwa mambo yamekuwa yakibadilika kila wakati.
Kwa upande wa wakuu wa Idara na Vitengo walionesha kufurahishwa na maudhui ya kitabu hicho kutokana na namna kilivyokidhi mahitaji ya changamoto za kilimo hasa mitaala katika vyuo vya Kilimo ambayo Wizara inaendelea na mchakato wa kuibadilisha.
Aidha Prof Tumbo ameendelea kusema kwamba kitabu hicho kinachoelezea namna ya kuongeza uzalishaji katika ardhi ''increasing production from the land" kinaweza kutumika kwa walimu, wanafunzi na watunga sera katika kuleta mabadiliko kwenye sekta hiyo.
hata hivyo Prof. alimalizia kwa kusema kwamba kitabu hicho kimegusa mambo mengi yakiwemo masoko ya mazao ya kilimo, upatikanaji wa fedha na mikopo kwa wakulima wadogo na jinsia katika kilimo hivyo ameshauri kwa kila mtaalamu wa wizara kupata nakala ya kitabu hicho ambapo zaidi ya vitabu 28 viliweza kununuliwa hapohapo.