Skip to main content
News and Events

KATIBU MKUU KILIMO MHANDISI MTIGUMWE AKABIDHIWA RASMI TUME YA TAIFA YA UMWAGILIAJI

Katika kuongeza ufanisi kwenye matumizi ya umwagiliaji katika kilimo kama sehemu ya utekelezaji wa Programu ya kuendeleza sekta ya kilimo awamu ya pili (Agricultural Sector Development Programme -Phase Two -ASDP II) rasmi Katibu Mkuu wa Wizara ya kilimo Mhandisi Mathew Mtigumwe amekabidhiwa Tume ya Umwagiliaji na katibu Mkuu wa wizara ya maji Prof Kitila Mkumbo.
 
Uamuzi huo wa Tume ya umwagiliaji kuhamishiwa wizara ya kilimo unalenga kuiwezesha wizara yenye dhamana ya sekta ya maji kudhibiti matumizi ya maji katika umwagiliaji bila kuwa na mgongano wa kimajukumu.
 
Imeelezwa kuwa sekta ya umwagiliaji ndiyo inayoongoza kwa matumizi ya maji hapa nchini  ambapo kwa sasa kiwango cha matumizi ya maji kwa ajili ya umwagiliaji kinakadiriwa kuwa mita za ujazo milioni 10,309 kwa mwaka ambacho ni sawa na asilimia 83.6 ya matumizi ya maji yote hapa nchini.
 
Kufuatia uamuzi huu wa serikali Tume ya umwagiliaji sasa itawajibika kiutawala kwa katibu Mkuu wa wizara ya kilimo na hivyo jina la wizara ya maji kubadilika na kuwa wizara ya Maji.
 
Katika kutekeleza maamuzi ya serikali ya kuhamishia wizara ya kilimo jukumu la umwagiliaji, leo tarehe 10 Octoba 2018 Katibu Mkuu wa wizara ya kilimo Mhandisi Mathew Mtigumwe na Katibu Mkuu wa wizara ya maji Prof Kitila Mkumbo wamefanya makabidhiano ya nyaraka muhimu kuhusu Tume ya Umwagiliaji zikiwemo sera ya umwagiliaji, Sheria ya umwagiliaji, na mpango kabambe wa Umwagiliaji (Revised National Irrigation Master Plan).
 
Utekelezaji wa maamuzi ya serikali kuhamishia jukumu la umwagiliaji kwenda wizara ya kilimo utaendelea kutekelezwa hatua kwa hatua katika mwaka wote huu wa fedha 2018/2019 na utakamilika kwa marekebisho ya Hati ya mgawanyo wa majukumu ya wizara ya Maji na Wizara ya kilimo.