Skip to main content
News and Events

WAZIRI HASUNGA ATEMBELEA KIWANDA CHA MBOLEA MINJINGU

Waziri wa kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) tarehe 18 Aprili 2020 ametembelea kiwanda cha mbolea cha Minjingu (Minjingu Mines and Fertilizer Ltd) kilichopo katika eneo na Kata ya Minjingu Mkoani Manyara ambapo pamoja na mambo mengine amejionea hali ya uzalishaji wa mbolea asilia ya kupandia aina ya Minjingu.

Mhe Hasunga ameshuhudia uzalishaji ukiwa umeongezeka kufikia Tani 100,000 kwa mwaka ambapo uongozi wa kiwanda hicho umetii agizo la Waziri Mkuu la kuwasihi kuboresha teknolojia ili kuzalisha Tani zaidi ya 150,000 ambazo zitaongeza kiwango cha upatikanaji wa mbolea hapa nchini kwwani bado upo chini kuliko mahitaji

Sambamba na hayo pia Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga ametoa mwito kwa uongozi wa kiwanda hicho cha mbolea Minjingu (Minjingu Mines and Fertilizer Ltd) kutoa elimu kwa umma juu ya ubora na umuhimu wa mbolea hiyo ya kupandia.

Mbolea hiyo inatokana na miamba inayochimbwa katika eneo la Minjingu Mkoani Manyara ambayo husagwa na kufungashwa kwenye kiwanda kilichojengwa katika eneo hilo. Mbolea ya Minjingu imeboreshwa kwa kuongezwa virutubisho vya Nitrogen, Salfa, Magnesi, Zinki na Boron (N, S, Mg, Zn, na B). 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda cha Mbolea cha Minjingu (Minjingu Mines and Fertilizer Ltd) Ndg Pardeep Singh Hans (Tosky) ameiomba serikali kupitia wizara ya kilimo kuwaruhusu maafisa ugani kote nchini kupatiwa mafunzo maalumu yatakayowaimarisha ili waweze kuwa sehemu ya kuitangaza mbolea bora ya Minjingu ambayo inazalishwa nchini.

Alisema kuwa serikali inapaswa kutazama upya utozaji wa VAT kwa wazalishaji wa bidhaa mbalimbali hapa nchini kwani tozo ya VAT wanayotozwa ni kubwa huku waagizaji wa mbolea nje ya nchi wao wanaingiza pasipo tozo kama hiyo.

Aidha, alisema kuwa tayari makala za vipindi vya Redio, Televisheni na Magazeti mbalimbali zimeanza kuandaliwa kwa ajili ya kuelimisha wakulima juu ya umuhimu wa mbolea hiyo ya Minjingu ambayo ni bora kuliko mbolea nyingine yoyote nchini na nje ya nchi.

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga amesema kuwa serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Mhe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli imejidhatiti katika viwanda, hivyo inathamini bidhaa zinazozalishwa na viwanda vya ndani.

Takribani asilimia 80 ya Watanzania ni wakulima. Shughuli hiyo ndiyo inawaingizia kipato ili waweze kukidhi mahitaji yao muhimu, ikiwamo kusomesha watoto wao, kugharamia matibabu na kadhalika.

Hata hivyo, wengi wamejikuta wakiishia kupata mazao yanayowatosha kwa chakula tu – bila ziada, huku wengine wakiishia kutupa nguvu na muda wao bure, hata hivyo Wizara ya Kilimo imeanzisha usajili wa wakulima ili kuwatambua na kuongeza ufanisi wa namna ya kuwahudumia, kadhalika kuanzisha bima ya Mazao ili wakulima wanapokumbwa na kadhia ya mavuno kidogo wawe na ahueni ya kulipwa kutokana na kuwa na bima.

Hali hiyo inatokea licha ya kulima eneo kubwa la ardhi ambalo kimsingi lingepaswa liwapatie chakula cha kutosheleza mahitaji yao katika familia pamoja na kupata ziada ambayo kama ingeuzwa ingewasaidia kwa mahitaji mengine muhimu.

MWISHO