DKT. OMAR ASHIRIKI KUSHEREHEKEA MIAKA 20 YA TAHA

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo anayesimamia Maendeleo ya Mazao na Usalama wa Chakula, Dkt. Hussein Mohamed Omar amesema kuwa Vituo vya Kukusanyia Mazao ya Horticulture vinaendana kuwa suluhisho kwa wakulima wa parachichi katika kupata huduma za usimamizi wa ubora, uhifadhi wa muda mfupi na maandalizi ya usafirishaji wa mazao yao kwenda sokoni, hasa masoko ya nje.
Amesema hayo tarehe 8 Mei 2025 Mkoani Njombe ikiwa ni sehemu ya kusheherekea Miaka 20 ya Taasisi ya Wakulima wa Mbogamboga na Matunda (TAHA), na kuongeza kuwa vituo vitasaidia kupunguza upotevu wa mazao, kuboresha ubora, na kuongeza thamani ya bidhaa katika masoko ya Kimataifa.
Naibu Katibu Mkuu Dkt. Omar ametoa wito kwa wakulima wote wa Mkoa wa Njombe na Mikoa ya jirani kutumia vyema fursa hiyo kwa kuwa vituo vipo kwa ajili yao.
“Shirikianeni na TAHA na wadau wengine ili kuhakikisha kuwa mavuno yenu yanapata thamani inayostahili. Nitoe wito kwa Viongozi wa Serikali za Mitaa na Halmashauri kushirikiana kikamilifu katika kulinda na kuendeleza miundombinu hii,” amesema Dkt. Omar.